Wednesday, 27 November 2013

David buruan
city no one
                                        picha zote kwa hisani ya David Buruan.
    Katika michezo iliyochezwa ya ligi kuu ya Vodacom msimu huu,mechi inayosemekana kwamba ilikua ni nzuri kuliko zote ni kati ya Azam na Mbeya City iliyochezwa katika uwanja wa Azam chamazi Dar.
            Inakumbukwa na wengi  kutokana na ubora wa mchezo ulioonyeshwa na timu zote mbili, kila timu ilionyesha kiwango cha hali ya juu sana kiasi hata sare iliyopatikana ya magoli 3-3 iliwaridhisha mashabiki wote.

       Katika mchezo huo, nyota wa mchezo kwa upande wa Mbeya  City alikua ni golikipa wa timu hiyo, David Buruan, kwani pamoja na kufungwa magoli matatu lakini aliokoa magoli mengi mno. Aliokoa mara mbili akiwa uso kwa uso na mshambuliaji hatari wa timu hiyo John Boco,akaokoa mara moja akiwa anatazamana na Joseph Kimwaga, na hizo zote washambuliaji hao walikua wamewapita mabeki wote au kwa kuwafikiria wameotea au kupigiwa pasi nzuri za mwisho,  lakini David aliweza kuwasoma na kuingia ndani na kucheza kama mlinzi wa mwisho na kuokoa hatari zote hizo.

                Hata faulo iliyowapatia Azam goli la kwanza, alikua ametoka na kwenda kumkabili Joseph Kimwaga aliyewachomoka mabeki wa City na bahati mbaya wakati akijaribu kuokoa akaushka mpira na kuzaa hiyo faulo.
              David alizaliwa mkoani Kigoma na kupata elimu yake mkoani Iringa,alianza kucheza mpira toka akiwa katika shule ya msingi Wilolesi mkoani Iringa na kwa vile kipaji chake hakikujificha aliweza kuchukuliwa mara kadhaa na timu  za mitaani na baadae akachukuliwa kabisa na timu ya Polisi Iringa.
        Na wakati akiwa Polisi Iringa, timu ya Simba ilifanya ziara mkoani Iringa na wakacheza na Polisi, na David akaaminiwa kua ni kipa katika mchezo huo na akafanya vizuri sana. Na hiyo ndio ilikua mechi yake kubwa ya kwanza.

             Baada ya hapo akachukuliwa na timu ya Tanzania Prisons,  huko akacheza kwa mafanikio makubwa hadi akachaguliwa kua ni kipa bora wa ligi kuu ya Vodacom msimu wa  2012/2013.
       Na timu ya Mbeya City ilipopanda daraja, kocha wa timu hiyo Juma Mwambusi aliamua kumchukua na kuwa ndio kipa namba moja wa timu hiyo.

         Na katika michezo yote aliyocheza ya ligi kuu msimu huu ameonyesha kiwango kikubwa na kumfanya awe ni mmoja kati ya makipa wazuri hapa Tanzania, ana uwezo mkubwa sana wa kuwasoma maadui na kuwapanga mabeki wake,na mara nyingi anaanzisha move haraka  pale wanapokua wameshambuliwa na akiudaka mpira anajua mahali pa kuupeleka. Pia ni mzuri sana kucheza krosi na mipira ya adhabu,hivyo kuwafanya walinzi  wake kutulia kila anapokua golini.

      Alikua ni kikwazo siku Mbeya City walipopambana na Yanga jijini Mbeya na kutoka sare ya 1-1, na akaonyesha kiwango cha juu walipocheza na Simba jijini Dar es salaam na  hata katika mchezo mgumu na Tz Prisons jijini Mbeya alikua katika kiwango bora sana cha mchezo.

       Kwa kiwango alichokionyesa katika misimu hii miwili, alipokua na Tz Prisons na sasa Mbeya City, siwezi kuja kushangaa siku atakapochukuliwa katika timu ya taifa ya Tanzania, na  nina uhakika akichukuliwa tu lazima atakua ni Tanzania one, na hatoki tena……

No comments:

Post a Comment