Sunday, 16 February 2014

Mbeya city walivyopambana na simba

 Mbeya City wamefanikiwa kutoka sare ya goli moja kwa moja na timu ngumu ya Simba iliyocheza kwa kiwango cha juu sana kuonekana hivi karibuni. Katika mchezo huo Simba walionekana kujaribu kumiliki kila idara na kuwafanya Mbeya City muda mwingi kujitahidi  kuharibu mipango ya Simba.

     Mchezo huo ulikua ni wa kiufundi zaidi na sifa za mwanzo ziwaendee makocha wa timu zote mbili kwa jinsi walivyoingia katika huo mchezo.
      Kocha Juma Mwambusi alibadili kidogo aina ya uchezaji wa timu yake, pale alipomuanzisha Hemed Kibopile acheze kama beki wa kushoto na Hassan Mwasapili asogee mbele  ili kuongeza idadi ya viungo na aweze mara kwa mara kurudi nyuma kusaidia walinzi,  kazi ambayo aliifanya kwa ufanisi mkubwa. Kwa hiyo Mbeya City walikua na viungo watatu, Mazanda, Matogoro na Mwasapili, ingawa hata Deus Kaseke nae alikua akiingia ndani kujaribu kuwasaidia viungo.
MASHABIKI WAKIGOMBEA TIKETI 
      Kwa upande wa Simba, walimuweka mshambuliaji mmoja tu Amisi Tambwe na mabeki halisi waliocheza walikua ni wawili, Josef Owino na Don Musoti,  hivyo wachezaji saba  waliobaki walikua ni viungo,  Henry Josef, Wiliam Lucien,  Said Ndemla, Amri Kiemba, Mkude, na hata Singano na Chanongo pia nao ni  viungo washambuliaji, na kwa jinsi jana wachezaji wa Simba walivyocheza kila mmoja alikua katika form ya hali ya juu sana na kuwafanya Mbeya City wacheze kwa nguvu zaidi ili kuweza kuwahimili.
MASHABIKI WA MBEYA CITY
         Jonas Mkude na Said Ndemla walifanya kazi ngumu sana ya kumzuia Steven Mazanda asianzishe mashambulizi, ingawa mara kadhaa alifanikiwa  kuwatoka na kupiga pasi kwa washambuliaji wake. Anton Matogoro alikua na kazi ya  kucheza na Amri Kiemba, hivyo muda mwingi wa mchezo alicheza chini ili aweze kumkaba Kiemba na wenzake waliokua wanakuja kila mara, ana mapafu ya ajabu sana Matogoro, na alicheza vizuri mno.
      Mmoja wa wachezaji walionivutia katika michezo miwili wa Mbeya City na Mtibwa na pia huu wa Simba ni Hemed Kibopile, ni mlinzi mzuri mno na anatumia akili na nguvu kila inapobidi, alicheza vizuri sana kumzuia Singano wa Simba, hadi alipopewa kadi ya njano na kocha kumuondoa ili kuepusha kadi nyingine ya njano. Aliweza kuhakikisha Singano hana madhara makubwa, ukichukulia Singano alivyo mzuri, hiyo ni kazi kubwa sana na aliifanya kwa ufanisi.
SHABIKI WA MBEYA CITY
     John Kabanda alicheza kwa tahadhari kubwa  kwani Chanongo alikua katika kiwango kizuri  na alikua akitaka kulazimisha kupita upande wa Kabanda, mpambano wao ulikua ni mzuri  kuutazama, ingawa baadae Chanongo alichoka na kuanza kupoteza umakini hadi akatolewa. Kabanda kama kawaida yake alipiga krosi kadhaa langoni mwa goli la Simba lakini nyingi ziliokolewa na walinzi.
         Kazi ilikua ni kwa Amisi Tambwe na Deogratius Julius, Tambwe alikua hatari sana na alipata nafasi kadhaa ambazo hakuzitumia vizuri ingawa alikuja kufunga goli lakini Deo alimdhibiti na kumfanya Tambwe mara nyingi kucheza kwa hasira. Deo alikua katulia mno na kuokoa kwa umakini mkubwa  hivyo kuweza kuhimili misukosuko yote iliyokua ikija langoni mwao.
           Yusuf Abdallah alikua akiosha  hatari nyingi  zilizokua zikija langoni na  ni yeye alliyekua akipambana na hatari zote zilizowapita mabeki wa pembeni na hata zilizopita katikati, ni mmoja kati ya mabeki bora sana hapa Tanzania.
   Hassan Mwasapili alicheza vizuri alipokua kiungo, lakini baadae aliporudi kucheza nafasi aliyoizoea ya beki wa kushoto alIcheza vizuri zaidi, kwani walianzisha tena kombinesheni yao na Deus Kaseke na kufanya mashambulizi kadhaa dakika za mwisho za mchezo.
MASHABIKI
        Deus Kaseke alicheza sana ndani tofauti na michezo mingi alivyozoeleka kucheza, hiyo inatokana na Simba kua na viungo wengi hivyo ikabidi aingie ndani zaidi kuwasaidia viungo wake, na alikua hatari kila mara anapopata mpira, alipeleka mipira kadhaa kwa washambuliaji wake na aliweza kuwasaidia vizuri viungo wa timu yake. Mara nyingi alifanikiwa kumtoka Lucien  na kupiga hiyo mipira katikati.
           Paul Nonga na hata Mwagane Yeya walikua na kazi nzito ya kupambana na walinzi warefu wa Simba kina Josef Owino na Musoti, ingawa ilionekana kuwakaba Nonga na Yeya ni kazi ngumu na inayohitaji ujasiri, Musoti na Owino walijitahidi kupambana hadi dakika ya mwisho.
MAMIA YA MASHABIKI WALIOJITOKEZA
     Kwa ujumla mchezo ulikua ni mzuri na wa kiufundi zaidi, viungo wa Simba walicheza kwa nguvu na akili sana hivyo kuwafanya wachezaji wa Mbeya City kutumia nguvu zaidi ili kuweza kuwazima Simba, na kikubwa Mbeya City wanacheza kwa ushirikiano kila idara ndio maana walifanikiwa,  kwani hadi mchezo unakwisha Mbeya City moja na Simba moja.
           

        PICHA NA MWANDISHI JUNIOR,IMEANDIKWA NA ABDUL SUDI, MBEYA

No comments:

Post a Comment